Print this page

“Yesu alipowaona makutano, aliwahurumia…”

Na Pd. Gaston George Mkude

Amani na Salama!
Injili ya leo, tunakutana na Yesu mbele ya makutano, waliokuwa wamechoka na kutawanyika. Makutano si tu wanawakilisha watu wa nyakati zile za Yesu, bali hata katika siku zetu leo hii.
Ni watu wangapi leo wanapitia magumu na mahangaiko, pamoja na mateso ya kila namna, labda hata baadhi yetu tumechoka, na kutawanyika kama kondoo tusio na mchungaji.
Wangapi leo wanaishi maisha yenye kila majeraha na maumivu! Wangapi leo wamechoka kimwili, kiakili na hata kiroho, kiasi cha kutawanyika na hata kutangatanga kiimani.
Wapo wanaokwenda kila siku, kwa wanaojiita mitume na manabii, na wengine kwa waganga wa kienyeji na wapiga ramli! Yesu anamuona kila mmoja wetu, na moja tu kutoka kwake, anatuhurumia!
Labda mara nyingi tunajiuliza, kwanini Mungu aliye upendo na huruma, anaruhusu wana na watoto wake tupitie magumu kiasi hicho?
Je, Mungu hawezi kutukinga na mateso na magumu? Au je, Mungu hatupendi hata anatuacha tukipitia kikombe hicho cha mateso na mahangaiko?
Ni maswali msingi na ya haki kabisa, kutuingiza katika tafakari ya fumbo la mateso, katika maisha ya ufuasi wetu.
Ni katika Injili ya leo, tunaona Yesu anapokutana na makutano wale, hata anapokutana nasi katika hali ngumu na taabu, anajawa na moyo wa huruma.
Yesu alipowaona, aliwahurumia! Huruma kama alivyokuwa anatukumbusha daima, hayati Baba Mtakatifu Fransisko, ndio haswa sura na utambulisho halisi wa Mungu wetu.
Mungu ni upendo na huruma! Papa Fransisko daima alipenda kurudiarudia na kusema ni sisi tunaochoka kuikimbilia huruma na upendo wa Mungu, kwani Mungu kamwe hachoki kutuhurumia na kutukumbatia tena na tena!
Shime katika kuikimbilia huruma na upendo wa Mungu! Jina na utambulisho wa Mungu ni Huruma!
Nabii Isaya anapotambulisha wema na huruma ya Mungu, anajaribu kutuonesha Mungu anatupenda zaidi ya mama anavyopenda watoto wake.
Sisi ni watoto wa Mungu kwa nafasi ya kwanza, na hivyo Mungu kwetu anajifunua kama upendo na huruma. (Isaya 49:14-16).

Rate this item
(0 votes)
Japhet

Latest from Japhet