Login to your account

Username *
Password *
Remember Me

Create an account

Fields marked with an asterisk (*) are required.
Name *
Username *
Password *
Verify password *
Email *
Verify email *
Captcha *
Reload Captcha

RUVUMA

Na Mwandishi wetu

Naibu Waziri Nishati, Judith Kapinga amesema kwa Serikali imetenga takribani Shilingi bilioni 4.6/- kupeleka umeme kwenye maeneo ya migodi mkoani Ruvuma.
Kapinga (pichani) aliyasema hayo wakati akizindua Kituo cha Mauzo ya Makaa ya Mawe ya kampuni ya Market Insight Limited (MILCOAL), inayojihusisha na uchimbaji, uuzaji na usambazaji wa makaa ya mawe, Wilaya ya Mbinga mkoani Ruvuma.

SIMANJIRO

Na Mwandishi wetu

Wachimbaji wa madini ya Green Garnet eneo la Lemshuku, Kata ya Komolo Wilayani Simanjiro Mkoani Manyara, wamelalamikia kwa Waziri wa Madini, Anthony Mavunde juu ya changamoto ya ukosefu wa maji, nishati ya umeme na kuwa na ubovu wa barabara.
Mmoja wa wachimbaji madini ya Green Garnet, Mkurugenzi wa Kampuni ya Chusa Mining Ltd, Joseph Mwakipesile alisema hayo wakati akizungumza na Waziri wa Madini, Anthony Mavunde baada ya kutembelea machimbo ya Lemshuku.
Mwakipesile alisema kuwa huduma ya maji ni changamoto kubwa kwenye machimbo ya Lemshuku, na hakuna nishati ya umeme, hivyo kushindwa kufanya uchimbaji kwa uhakika.
“Maji yanafuatwa umbali wa kilomita 17 kutoka kijiji cha Komolo hadi hapa machimboni, na tulikuwa na kisima cha maji, ila hivi sasa tuna maji tunafuata mbali, na pia barabara ni mbovu,” alisema Mwakipesile.
Kwa upande wake Mwenyekiti wa Chama cha Wachimbaji Madini (MAREMA), Tawi la Lemshuku, Swalehe Abdalah aliiomba Serikali kufanikisha utatuzi wa changamoto hizo ili waweze kufanya shughuli za uchimbaji kwa uhakika.
“Tunakushukuru Waziri Mavunde kwa kufika Lemshuku na kuona mazingira ya hapa Lemshuku, tunaomba serikali imalize vikwazo tulivyonavyo ili tufanye kazi vyema,” alisema Swalehe.
Akijibu malalamiko hayo, Waziri Mavunde alisema atakutana na Mawaziri husika ili kuhakikisha changamoto hizo zinafanyiwa kazi kuwawezesha wachimbaji hao waweze kufanya kazi zao ipasavyo, na Serikali iongeze mapato.
Waziri Mavunde alisema miundombinu ikiboreshwa na changamoto zikipatiwa ufumbuzi, Watanzania hao watatajirika kwa kupata fedha nyingi, na serikali itaongeza mapato kupitia kodi.
Hata hivyo, ili kumaliza changamoto ya ukosefu wa huduma ya afya, ameendesha harambee ya ghafla ya ujenzi wa zahanati na kupatikana Sh23 milioni matofali 3,000 na mifuko 185 ya saruji
Aliuagiza uongozi wa mamlaka ya maji safi na usafi wa mazingira vijijini (RUWASA) Wilaya ya Simanjiro, kuhakikisha pampu iliyozama kisima cha maji Lembole inatolewa ili wachimbaji wapate huduma wakati wakisubiri mradi mkubwa wa maji.
Akizungumza kuhusu mawasiliano alisema kwamba atazungumza na waziri husika ili mnara wa simu ufungwe kwenye machimbo hayo na hivyo mawasiliano yapatikane.
Naye Mkuu wa Wilaya ya Simanjiro Fakii Lulandala alisema kuwa hii ni mara ya kwanza Waziri wa madini kufika kwenye machimbo ya Lemshuku, hivyo Waziri Mavunde anapaswa kupongezwa.
Naye Rais wa Shirikisho la Vyama vya Wachimbaji Madini nchini, Femata John Bina alisema Waziri Mavunde ni kiongozi wa pori kwa pori asiyekaa ofisini ndiyo sababu amefika Lemshuku huku Mwenyekiti wa chama cha mabroka Tanzania (Chamata) Jeremiah Kituyo amewaasa wanunuzi wa madini kukata leseni ili waweze kuwa huru na biashara yao.
Mbunge wa Simanjiro Christopher Ole Sendeka naye alisema wachimbaji hao wa Lemshuku wakitatuliwa changamoto zao watanufaika ikiwemo wachekechaji.

LINDI

Na Mwandishi wetu

Baraza la Uwezeshaji Wananchi Kiuchumi, (NEEC) limewataka viongozi wa Mkoa wa Lindi, kutengeneza mkakati kabambe utakaozuia mimba za utotoni kwa wasichana kuwakatiza masomo na kuzima ndoto zao.
Kauli hiyo ilitolewa na Katibu Mtendaji wa baraza hilo, Beng’i Issa wakati baraza hilo lilipozindua programu ya Imarisha Uchumi na Mama Samia (IMASA)mkoani humo.
“Mkoa huu una matatizo ya wasichana kuacha masomo, hata wakiwa wamefaulu kujiunga na shule za sekondari hawaendi na inakadiriwa asilimia 30 yao hukatisha masomo kutokana na mimba za utotoni…mimba za utotoni zinakatisha ndoto za kiuchumi za wasichana,”alisema Beng’i.
Alisema programu ya IMASA imekuja kuwezesha Makundi ya kinamama, vijana, na makundi maalum. Hivyo makundi ya vijana yakipata elimu, ni nyenzo kubwa ya kufikia malengo yao ya kiuchumi na ukizingatia mkoa huo una fursa nyingi za kiuchumi.
Beng’i alisema kwamba mkoa huo wananchi wanajishughulisha na kilimo cha korosho,alizeti,uvuvi, mazao ya mwani, hivyo programa hiyo itashirikiana na mkoa huo kuweka vipaumbele ili kuandaa programu kwa ajili ya uwezeshaji wake.
Alisema pia kuwa program ilipokelewa vizuri mkoani humo na wananchi walitamani sana programu ianze haraka, na washiriki wengi walikuwa ni wafanya biashara, wakulima, wakulima wa kuongeza thamani mazao, na madalali wa kilimo.
Aidha, aliutaka uongozi wa Mkoa huo kuendelea na programu zao za kawaida katika kilimo cha korosho, ubanguaji korosho kuongeza thamani mazao na uvuvi, na zile za uwezeshaji za asilimia kumi na kuendelea, kufuata maelekezo ya serikali.
Naye Katibu wa Shirikisho la Watu Wenye Ulemavu Manispaa ya Lindi, Zuhura Meza alisema anamshukuru Rais Dk. Samia Suluhu Hassan kwa kuanzisha programu hiyo ambayo imekuja kuwainua kiuchumi wanawake kupitia mafunzo ya ujasiriamali na uwezeshaji watakaopewa.
“Nikirirudi nyummbani naenda kuwaelimisha watu wenye ulemavu, wale ambao hawajajisajili na programu ili nao waende kujisajili ili kupata fursa ya mafunzo na uwezeshaji,” alisema.
Naye Mkulima wa Mwani kutoka Kata ya Lindi Mjini ya Kitumbi, Kwela, Manispaa ya Lindi, Rukia Selemen alisema yeye ni mkulima na mchakataji wa bidhaa za mwani. Anashukuru ujio wa program hiyo kufika katika manispa yao kutoa elimu ya ujasiriamali na itamwezesha kufanya vizuri zaidi.
Mjasiriamali toka Kilwa Masoko Fatuma Juma alisema anajishughulisha na usindikaji wa mazao mbalimbali, yakiwemo ya maziwa (yogati), juice ya mwani na anatengeneza bidhaa za urembo kama nguo, na alidai kwa kusema kuwa programu hiyo imewaingiza katika mfumo na hivyo kufanya kazi kwa ubora.

DAR ES SALAAM

Na Laura Chrispin

Askofu Mkuu Mstaafu wa Jimbo Kuu Katoliki la Dar es Salaam, Mwadhama Polycarp Kardinali Pengo amewaasa Waamini kutambua kwamba ufukara na umaskini isiwe ni sababu ya wao kuikana imani.
Kardinali Pengo (pichani), alitoa wito huo hivi karibuni wakati akitoa homilia yake katika Adhimisho la Misa Takatifu ya Sakramenti Takatifu ya Kipaimara, iliyoadhimishwa Parokia ya Bikira Maria wa Fatima-Msimbazi, jimboni Dar es Salaam.
“Kuna baadhi ya watu kutokana na umaskini na ufukara wao, wamediriki kuikana imani yao ili mradi wapate baadhi ya vitu walivyokuwa wakihitaji,”alisema Kardinali Pengo.
Aliendelea kusema, “Nanyi Waamini na watoto mnaopokea Sakramenti ya Kipaimara, inawapasa kufahamu, hata Yesu alikuwa ni mtu fukara zaidi, lakini bado aliishi katika imani…hivyo basi nanyi inawapasa  kuishi katika imani hiyo hiyo aliyokuwa nayo Yesu Kristo mwenyewe, ikiwa kama kielelezo na mfano bora wa maisha ya Mkatoliki.”
Kardinali Pengo alisema wanatakiwa kutambua kuwa Mwenyezi Mungu hana shida na fedha za mtu yeyote, bali anahitaji watu waongoke na kuiamini Injili.
Inawapasa kufahamu “maskini anayeongelewa na Muinjili Mathayo, si maskini wa mavazi, malazi au makazi, bali ni maskini yule asiyelifahamu Neno la Mungu”
Kardinali Pengo alisema kwamba Yesu Kristo alikuja duniani kwa kazi moja ya kuwahubiria Injili watu maskini na kuwakomboa wanadamu.

Askofu Msaidizi wa Jimbo Kuu Katoliki la Dar es Salaam, Mhashamu Stephano Musomba-OSA katika Kigango cha Mtakatifu Antoni wa Padua – Nyeburu, Parokia ya Mtakatifu Yohane Paulo II – Buyuni, Adhimisho la Misa Takatifu ya Somo wa Kigango hicho. (Picha na Michael Ally)

DAR ES SALAAM

Na Israel Mapunda

Naibu Waziri wa Uchukuzi, David Kihenzile amesema kuwa Serikali itaendelea kushirikiana kwa karibu na Sekta Binafsi kwa kuweka mazingira wezeshi, ili kuhakikisha Sekta ya anga inakua na kuchangia ukuaji wa Pato la Taifa.
Waziri Kihenzile (pichani), alisema hayo jijini Dar es Salaam baada ya kutembelea anga ya kampuni ya Ndege ya Precision, kukutana na kuzungumza na Wakurugenzi watendaji wa Coastal Aviation na Flightlink.
Katika ziara yake hiyo, Naibu Waziri Kihenzile alisema kwamba uwekezaji unaofanywa na Serikali kwenye eneo la kuboresha miundombinu ya viwanja vya ndege, utakuwa na matokeo makubwa pale ambapo sekta binafsi pia itawekeza katika ununuzi wa ndege.
Kihenzile aliongeza kuwa Serikali ipo katika hatua mbalimbali ya kufanya maboresho kwenye sera ya Uchukuzi na Sheria ya Mamlaka ya Viwanja vya Ndege, kwa lengo la kuimarisha sekta ya usafiri wa anga.
Naye Mkurugenzi wa Precision, Patrick Mwanri alisema kwamba katika mpango kazi wake, imepanga kuongeza ndege ambazo zitakwenda sambamba na ongezeko la vituo ambavyo kampuni itakuwa ikitoa Huduma nchini.
Mkurugenzi Mwanri aliiomba Serikali kupitia Naibu Waziri Kihenzile, kuzisaidia kampuni binafsi za ndege kuweza kupata mikopo kupitia benki za ndani, ili kuziimarisha kwenye uendeshaji.
Naye Mkurugenzi Mtendaji wa Kampuni ya Flightlink, Kapteni Munawer Dhirani aliishukuru Serikali kwa kutekeleza dhamira yake ya kuweka mazingira mazuri ya sekta ya anga, na kuhakikisha makampuni binafsi yanaendelea kuwekeza kwa kununua ndege nchini.
Kapteni Munawer aliongoza kuwa  mazingira yaliyowekwa yameiwezesha Kampuni ya Flightlink kuweka mipango ya  kuongeza mtandao wa safari, ambapo mapema mwisho wa mwaka, Kampuni hiyo itaongeza kituo cha Mwanza.

DAR ES SALAAM

Na Laura Chrispin

Askofu Mkuu wa Jimbo Kuu Katoliki la Dar es Salaam, Mhashamu Jude Thaddaeus Ruwai’chi amewataka waimarishwa kuwa Manabii wa kweli na kusikiliza sauti ya kichungaji wanapoitwa na Mungu.
Askofu Mkuu Ruwa’ichi alisema hayo wakati wa Adhimisho la Misa Takatifu ya Sakramenti Takatifu ya Kipaimara iliyoadhimishwa katika Parokia ya Mwenyeheri Antonio Rosmini - Mpigi Magoe, jimboni humo.
“Muimarishwa unaitwa kuhubiri Habari Njema za Kristu, pamoja na kufanya mambo yaliyo mema na yenye kumpendeza Mungu, na si kuwa nabii wa uwongo,” alisema Askofu Ruwa’ichi.
Aliongeza kuwa zama za sasa zimekuwa na manabii wengi wa uongo, ambao lengo lao ni kudanganya, na si kutangaza Neno la Mungu.
Aidha, Askofu Mkuu Ruwai’chi alisema kuwa Mkatoliki aliyebatizwa, hapaswi kuwaamini manabii wa uongo, bali anatakiwa kuishi katika imani yake.
Aliwakumbusha Waamini kwamba manabii wa uwongo wamekuja kwa kazi ya kutafuta fedha tu, na si kwa ajili ya kuhubiri Neno la Mungu, akiwasisitiza kusimama imara katika imani yao.
“Nabii wa kweli hutokana na kusema ukweli, na siku zote maisha yao si rahisi, kwa sababu ndani yao mara zote kumejaa manyanyaso ya kusakamwa, ya kusutwa, pamoja na kudhulumiwa,” alisema Askofu Mkuu, na kuongeza,
“Hata katika Somo la Kwanza anazungumziwa Nabii Yeremia ambaye ni kati ya manabii mahiri zaidi katika Agano la Kale, ambaye mara zote alikuwa anawaambia watu wamrudie Mungu kutokana na mambo yao waliyokuwa wakitenda.
“Lakini, kwa sababu alikuwa ni nabii aliyesimama katika ukweli zaidi, watu hao walimkamata na kumuhukumu kifo, lakini ni kwa sababu Yeremia aliwataka watu wabadilike kwa kutubu ili yasije kujitokeza tena yale ya Sodoma na Gomora. Hiyo inaonesha fika ni kwa jinsi gani Manabii wa ukweli wanavyoteseka.”
Aidha, Askofu Ruwa’ichi aliwakumbusha Waamini kutubu na kuamini Injili, ikiwa kama ujumbe wa Yesu aliowaachia wanafunzi wake, akiwataka kutokufanya maamuzi ya haraka, bali wafikiri zaidi na kutenda ili baadaye wasije kujuta.
Aliwakumbusha Waimarishwa kuwa siku ya Ubatizo walizaliwa mara ya pili kama hekalu la Roho Mtakatifu, akiwataka watambue na wajiheshimu kwa kuuishi vyema wito wao.
Aliwasisitiza kushuhudia matendo makuu ya Mungu, akiwaasa kuwa kipaumbele ni kuzungumza habari njema kwa watu, na kuwakumbusha kutokuwa manabii waliokufa, wala manabii wasiokuwa na uthubutu.
Hata hivyo, Askofu Mkuu aliwataka wazazi na wasimamizi kuwa mfano bora wa kuigwa na watoto, kwa kuwasaidia kuishi vyema wito wao siku zote za maisha yao.

DODOMA

Na Mwandishi wetu

Mkuu wa Mkoa wa Dodoma, Rosemary Senyamule amewaasa wataalamu wa sekta za mifugo na uvuvi kupeleka na kufundisha teknolojia za sekta hizo vijijini, ili kuwapa elimu wafugaji kuhusu ufugaji wa kisasa, na hivyo kuleta tija.
Alisema hayo alipotembelea kwenye Maonesho ya Kilimo ya Kimataifa (Nane Nane) yaliyofanyika Kitaifa mkoani humo.

MOROGORO

Na Winfrida Kobelo-SJMC

Wakazi wanaoishi karibu na Hifadhi ya Hululu iliyopo Kata ya Bunduki, mkoani Morogoro wametakiwa  kuitunza hifadhi hiyo.
Kauli hiyo imekuja wakati huu Taifa linapoendelea na harakati za kukabiliana na changamoto za mabadiliko ya tabianchi, ambayo yamezidi kuwa tishio duniani kote.
Wakizungumza na gazeti  Tumaini Letu hivi karibuni, baadhi ya viongozi wa mazingira wa kata hiyo walisema kuwa kwa sasa wanatumia njia mbalimbali kudhibiti uharibifu wa hifadhi hiyo, ikiwemo kufanya doria za mara kwa mara.
Afisa Misitu wa Kata hiyo, Protches Elias alisema kwamba wamekuwa wakitoa elimu kwa wanakijiji, ili wahakikishe mazingira yanatunzwa, ikiwemo kutokuchoma moto katika misitu iliyomo ndani ya vijiji hivyo.
“Tumekuwa tukitoa elimu kwa vijiji na vitongoji kuhusiana na majanga ya moto pamoja na uanzishwaji wa vitalu vya miti, na upandaji miti. Pia tunafanya doria za mara kwa mara ili kukabiliana na vitendo vya uharibifu kama vile ukataji miti, kilimo na upitishwaji wa mifugo ndani ya hifadhi,” alisema Afisa Misitu huyo, na kuongeza,
“Suala lingine ni ulinzi na uimarishaji wa mipaka ya hifadhi kwa kufyeka na kusafisha mipaka ili miti iliyopo mpakani ikue vizuri na hivyo kuzuia majanga ya moto ambayo yanaweza kusababishwa na mashamba ya wenyeji yaliyo jirani.”
Akizungumzia changamoto wanazokumbana nazo katika kuitunza hifadhi hiyo, Afisa Misitu huyo alisema kuwa changamoto hizo ni pamoja na uhaba wa watumishi, na baadhi ya wananchi kufanya shughuli za kilimo katika maeneo ya pembezoni mwa hifadhi hiyo.
Naye Mwenyekiti wa Mazingira katika Kijiji cha Vinile kilichopo karibu na hifadhi hiyo ya Hululu, Paulo Joseph alisema kuwa wananchi ndio watunzaji namba moja wa hifadhi kutokana na kamati mbalimbali za mazingira ambazo zimeundwa kwa ajili ya kusimamia misitu na kupanda miti, kwani misitu ndiyo chanzo cha upatikanaji wa maji.
Hata hivyo, Mwenyekiti huyo aliwaasa wananchi kuendelea kutunza na kuyathamini mazingira kwa kuachana na tabia za kukata miti, kuchoma moto misitu, pamoja na kuharibu vyanzo vya maji, ili kuepuka madhara yatokanayo na mabadiliko ya tabianchi.
Kwa upande wake Veronica Mwenda, mmoja wa Wajumbe wa Kamati ya Mazingira katika Kata ya Bunduki, alieleza kuwa bado wanakumbana na changamoto za matukio ya uharibifu wa misitu, kama vile ukataji hovyo miti.
Naye mkazi wa Kijiji cha Maguruwe kilichopo Kata ya Bunduki, Josephina Christopher, alisema kuwa wameunda baadhi ya vikundi vya upandaji miti katika vitalu kwa ajili ya kutokomeza uhaba wa miti katika misitu hiyo.
“Kwa mfano, pale kijijini kwetu tumekuwa na baadhi ya vikundi mbalimbali mahsusi kwa kupanda miti, na hii ni kwa sababu tunaipenda hifadhi ya Hululu, maana ile ni hazina ya asili tunayojivunia,” alisema Josephina.
Aidha, hifadhi ya Hululu kwa jina lingine hujulikana kama Maporomoko ya Maji ya Hululu, na yana urefu wa sentimita 80 kutoka yanapotoka hadi yanapotiririka, yaliyopo ndani ya msitu wa hifadhi ya mazingira asilia ya Uluguru.

RUKWA

Na Lusungu Helela

Naibu Waziri, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Deus Sangu, amesema kuwa Serikali imepanga kutangaza jumla ya  ajira mpya  37, 616, huku ajira za kada ya Ualimu, Afya   na kada nyinginezo, ikiwemo kada ya Uhasibu  na Ugavi, zikiwa tayari zinaendelea kutangazwa, lengo likiwa ni kupunguza tatizo la upungufu wa watumishi nchini.
Sangu alisema hayo kwa nyakati tofauti wakati akizungumza  katika mikutano ya hadhara iliyofanyika katika vijiji vya Kitete, Laela, Kamsamba na Kavifuti vilivyopo katika  Halmashauri ya Wilaya ya Sumbawanga, mkoani Rukwa, ikiwa ni ziara yake ya  kwanza tangu alipouteliwa kushika  wadhifa huo.
Akizungumzia nafasi za ajira ya Ualimu ambazo tayari zimeshatangazwa na Sekretarieti ya Ajira kwenye ngazi ya mikoa kulingana na mahitaji ya mkoa husika,. Sangu alisema kuwa utaratibu wa kuwapata waalimu kwa mwaka huu umeanza kuwa wa tofauti ukilinganisha na ilivyokuwa katika miaka ya nyuma.
Alifafanua kuwa usaili huo umeanza kufanyika kwa kada ya Ualimu kwa sababu nafasi  za ajira za Ualimu  ni chache, ukilinganisha na idadi ya walimu wa shule ya msingi na sekondari waliohitimu vyuo mbalimbali hapa nchini, ambapo zaidi ya waalimu 100,000 wapo mitaani wakiwa hawana ajira.
Alisema kuwa Serikali imekuja na uamuzi huo ili kuchagiza dhana ya ushindani kwa lengo la kuhakikisha kila mwenye sifa stahiki, anapata ajira katika mazingira aliyopo pasipo kulazimika kusafiri kwenda Dodoma au Dar es Salaam kwa ajili ya kufanya usaili.
Kufuatia hatua hiyo. Sangu alitoa wito kwa vijana waliohitimu vyuo mbalimbali hapa nchini kuchangamkia nafasi hizo za ajira, huku akiwataka wajiandae ipasavyo kwa ajili ya usaili huo, ikiwa ni mara ya kwanza kwa kada hiyo ya Ualimu kufanya usaili
Alitumia fursa hiyo kuwatoa wasiwasi wote walioomba nafasi hizo za Ualimu, huku akiwahakikishia kuwa Ofisi yake yenye dhamana ya kusimamia masuala ya ajira nchini, imejizatiti kuhakikisha mchakato huo wa kuwapata waalimu wenye sifa stahiki utakuwa huru na wa haki.