Dar es Salaam
Na Mwandishi wetu
Siku chache baada ya mshambuliaji wa Taifa Stars, Mbwana Samatta, kutangaza kustaafu kuichezea timu hiyo, Mamlaka husika zimeshauriwa kuingia makubaliano, na nchi zilizoendelea kisoka, kutusaidia kukuza vipaji vya vijana.
Akizungumza na Tumaini Letu katika mahojiano maalumu, beki wa zamani wa Taifa Stars, Bakari Malima, alisema kuwa njia pekee ya kuwapata kina Samatta wengi, ni kuhakikisha wachezaji wa timu za taifa za vijana, wanaong’ara kwa sasa hawapotelei mitaani, na badala yake wasaidiwe kwa kupelekwa kwenye nchi mbalimbali za Ulaya, ili miaka ya baadaye, wawe msaada mkubwa kwenye soka la Tanzania.
Alisema kwamba, Serikali kwa kushirikiana na Mamlaka za soka, hasa Shirikisho la Mpira wa Miguu nchini (TFF), wanapaswa kutengeneza mpango mkakati, wa kuhakikisha wanaingia makubaliano na baadhi ya nchi za Ulaya zilizoendelea kisoka, na kisha kuchukua baadhi ya vijana, kuwapeleka katika Ligi za vijana, na vituo vya vijana vya nchi hizo.
“Wanaweza kuchukua wachezaji wawili, watatu ama wanne, wakawa wanawapeleka katika nchi husika ya Ulaya, kwa mfano wakiingia makubaliano na nchi tano za Ulaya, kila nchi wanaweza kupeleka baadhi ya wachezaji, ili kupata uzoefu huko na baadaye, wanakuja kuusaidia mpira wetu,” alisema Malima.
















